Breaking News

Maumivu Wakati Wa Kukojoa



Maumivu wakati wa kukojaoa ni hali inayotokea kwa watu wengi ikisababishwa na magonjwa mbalimbali. Maumivu wakati wa kukojoa hujulikana kwa kitaalamu kama dysuria. Kati ya sababu kuu zinazosababisha maumivu wakati wa kukojoa ni maambukizi ya mfumo wa mkojo (Urinary tract Infection – UTI) hasa kwa wanawake na magonjwa ya zinaa

Maumivu Wakati wa Kukojoa Yanavyotokea 

Maumivu wakati wa kukojoa hutokana na kuchubuka kwa njia ya mkojo. Kuchubuka huku hutokea pale njia ya mkojo inaposhambuliwa na bakteria au kemikali na kuharibu ukuta wa juu wa njia ya mkojo hivyo huwa kama kidonda. Pale mkojo unapopita eneo hili basi unapata maumivu kama ya kuungua. Maumivu haya yanaweza kutokea wakati wote unakojoa, mwanzoni au mwishoni mwa kukojoa.

Kwa watoto wadogo, mara nyingi hulia wakati wanakojoa ikiwa wanapata maumivu kwani hawawezi kuongea.

Pia yanaweza kuambatana na dalili nyingine kama homa, kutokwa na usaha au uchafu sehemu za siri, kutokwa mkojo wenye damu damu, maumivu chini ya kitovu au maumivu ya ubavu (flanks). 

Sababu za Maumivu Haya

Maumivu haya hutegemea na chanzo cha ugonjwa unaoleta dalili hii. Baadhi ya vyanzo vya maumivu wakati wa kukojoa ni:

Maambukizi ya njia ya mkojo (UTI)

Ugonjwa huu huleta maumivu kama ya kuungua kwenye njia ya mokojo. Pia maumivu yanaweza kufika mpaka chini ya kitovu wakati wa kukojoa. Dalili nyingine zinazoweza kuambatana na hali hii ni homa, kukojoa mara kwa mara, kuhisi mkojo hauishi kwenye kibofu na maumivu ya mgongo.

Magonjwa ya zinaa

Magonjwa ya zinaa kama kisonono na klamidia huleta maumivu wakati wa kukojoa hasa kwa wanaume, maumivu haya huwa kama ya kuungua wakati mkojo unatoka. Dalili nyingine zinazoweza kuambatana na magonjwa haya ni kutoa uchafu kama usaha sehemu za siri, maumivu chini ya kitovu na homa.

Kichocho

Kichocho husababisha maumivu wakati wa kukojoa ikiambatana na kutoa mkojo wenye damu.

Magonjwa mengine yanayoweza kusababisha maumivu wakati wa kukojoa ni:
  • Mawe ya Figo (kidney stones)
  • Maambukizi ya ukeni (vaginitis)
  •  Saratani ya kibofu cha mkojo
  •  Kuchubuka kwa njia ya mkojo kutokana na ajali, kupigwa, kuendesha farasi au mazoezi mengine.
  •  Kuwekewa mpira wa mkojo (urinary catheter) au kuingizwa vipimo vya njia ya mkojo au kibofu (instrumentation of urethra or bladder).

vipimo

Vipimo vifuatavyo vinaweza kufanyika ili kujua chanzo cha maumivu wakati wa kukojoa.

  •  Kipimo cha uchunguzi wa mkojo (urinalysis)
  •  Kuotesha mkojo (urine culture)

Uchunguzi za mkojo na kuotesha mkojo huweza kuonesha kama kuna maambukizi kwenye njia ya mkojo. Pia mabaki ya mawe ya figo huweza kuonekana.

  •     Kipimo cha Ultrasound ya tumbo na kiuno (Pelvic and abdominal ultrasound).
Kipimo hiki huweza kuonesha matatizo ya kwenye figo ikiwemo mawe ya figo, uvimbe kwenye mfumo ya mkojo au maambukizi ya figo. Vipimo vingine kama X-ray au CT Scan vinaweza kufanyika kama dalili nyingine zikiashiria hivyo.

Matibabu

Maumivu wakati wa kukojoa ni dalili, hivyo matibabau huelekezwa kwa ugonjwa unaoleta tatizo hili. Maumivu haya yanaweza kutibiwa na kupona kabisa. Ikiwa mtu atapata tena maambukizi yaliyoleta dalili hii awali, basi maumivu haya yanaweza kujirudia tena.

Wahi kwenye kituo cha kutoa huduma za afya uonapo dalili kama hii haraka. Endapo dalili nyingine zinatokea kama damu kwenye mkojo, homa au maumivu ya kwenye ubavu usipoteze muda
    Endelea

No comments